Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Rizki Pemba Juma akiwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo Simai Mohammed Said, wakisalimiana na Wanafunzi wa Skuli ya Sekondari Unguja Ukuu Mkoa wa Kusini Unguja

Sekta ya Utalii ni moja ya sekta ambazo serikali ya Zanzibar imekuwa ikizitegemea katika ukusanyaji wa kodi, ni sekta ya Biashara, sekta ya Utalii, Viwanda, nyumba za kulala wageni na starehe yaani pamoja na sekta nyengine mbali mbali ambazo zinatambulika kwa mujibu wa sheria za nchi.

Licha ya sekta hizo na nyengine nyingi kuwa ni sehemu ya tegemeo la serikali katika ukusanyaji wa fedha ambazo hutumikwa kwa ajili ya kuleta maendeleo ya jamii, lakini kwa upande mwengine baadhi ya sekta hizo uwepo wake bila ya kuangaliwa vyema uendeshaji wake ni wazi kuwa zinaweza kuleta athari makubwa kwa jamii hasa watoto ambao ndio tegemeo la kesho.

Moja ya sekta hizo ni sekta ya Biashara ya nyumba za kulala wageni na starehe yaani Baa, hasa kwa zile Baa zinazoanzishwa pembezoni au karibu na makaazi ya wananchi au karibu ya shule hasa za watoto wadogo yaani shule za msingi za kati pamoja na Secondary.

Ni dhahiri kuwa pasi na usimamizi ulio bora wa uanzishwaji wa Baa athari kwa watoto kuacha masomo au kutofikia malengo yanahitajika katika upatikanaji wa elimu bora kwa watoto walio chini na umri wa miaka 18 wakiwamo wanaume na wanawake.

Pamoja na athari za baa kuwepo katika maeneo mengi lakini katika Makala haya nimeanagazia Mkoa wa Kusini Unguja, katika Wilaya ya Kusini ambapo kwa mujibu wa sensa ya watu na makaazi ya mwaka 2012 Wilaya ya Kusini Unguja ina jumla ya wakaazi 39,242 wakiwamo wanaume 19,342 na wanawake 19,900 .

Licha ya biashara hiyo kuwa kuna baadhi ya watu wanaikubali lakini wananchi walio wengi katika Wilaya hiyo pamoja na viongozi mbali mbali pamoja na wadau na wanaharakati wamekuwa wakizilalamikia kutokana na maadili ya watoto kuanza kupotea kidogokidogo.

Wazazi wazungumzia suala hilo

Baadhi wananchi wamesa ni jambo la kusikitisha sana kuona kila uchao katika Wilaya hiyo ongezeko la Baa maeneo yasiostahiki ikiwamo maeneo ya karibu na shule limekuwa linazidi, hali ambayo imeanza kuleta athari kwa watoto wao wadogo hasa wale walioanza kuoma shule.

Mmoja wananchi hao ambao hakupendwa kutajwa jina lake gazetini kutokana na sababu zake za msingi alisema baadhi ya watoto wao tayari wameanza kuathirika kitabia kutokana na uwepo wa Baa hizo, ziliomo maeneo ya karibu na makaazi pamoja na Shule.

Alisema baadhi ya watoto tayari wamebadilika wengine wameanza kujiingiza katika matumizi ya vinywaji vya ulevu na wengine wamo katika kundi vitendo vya ngono.

Alisema jitihada mbali mbali wameweza kuchukua ili kuona Baa hizo zinasimamishwa kazi lakini hadi sasa hakuna mafanikio yaliopatikana, licha ya kundi la watoto walio chini ya umri wa miaka 18 kuanza kubadilika kimaadili.

“Mtoto anakuanga anaenda shule kumbe hafiki shule anamalizia Baa, inasikitisha sana kwani wakati wowote watoto wanaweza kuathirika hata kiafya, tunaamini hali hii inaweza kuondoka pindi serikali ikachukua hatua madhubuti juu ya wamiliki wa Baa”alisema.

Kwa upande baadhi ya wanafunzi nao hawakunya nyuma kulisemea hilo, ambapo walidai kuwa ni ukweli kwamba uwepo wa baa maeneo ya karibu na Shule kunawaathiri sana kielimu kutokana na kelele zikiwamo za walevi pamoja mavazi ya wasichana wanaotumia baa hizo.

Wadau wazungumza

Mmoja wadau wakubwa wanaoguswa na kadhia hiyo ni Kaimu Mwalimu Mkuu wa Shule ya Kizimkazi Mkunguni, Mah-fudh Said Omar alisema licha ya jitihada kubwa wanayochukua juu ya ufundishaji wananafunzi lakini kuwepo kwa Baa hizo kunachangia kwa kiasi kubwa kutofikia malengo yao,akidai kuwa baadhi ya wanafunzi huacha kabisa kuendelea na masomo kutokana na kuathiriwa na Baa hizo.

Alisema kuwepo kwa baa hizo baadhi ya wanafunzi hushawishika kujiingiza katika vitendo viovu, ikiwamo unywaji ulevi pamoja na vitendo vya uasharati, hali inayochangiwa na wigo kutoka kwa watumiaji wa Baa hizo kijijini hapo.

“Kiukweli halii hii huchangia kushuka kwa kiwango cha elimu kwa wanafunzi wetu, hivyo ni vyema kwa taasisi husika kulitafutia ufumbuzi tatizo hili ili kuona vijana wetu wananufaika vema na elimu, pamoja na kuifanya shule yetu kupata matokeo mazuri ya mitihani”alisema.
 
Naye Mjumbe wa kamati kuu ya Wapinga Baa Zanzibar, Seif Omar Seif amefahamisha kuwa baa nyingi zilizopo nchini zipo karibu na makaazi ya watu jambo linalopelekea kuhatarisha usalama wa watoto.

Alisema wao kama wapinga Baa mara nyingi huchukua jitihada za kutoa elimu kwa jamii hasa katika kipindi cha utoaji wa leseni za Baa, kwenda Mahakani ili kupinga uwepo wa Baa hizo ila kinachotokea ni baadhi ya wananchi kushindwa kujitokeza kwa wingi katika kuweka pingamizi.

Alisema pindi wananchi wakiungana kwa pamoja hasa kwa kuweka pingamizi ya kupatiwa leseni, ni suluhisho kubwa la kusitisha Baa hizo, akidai kuwa kinyume chake wanaweza kutumia muda mwingi wa kulalamika bila ya kupata muafaka kwa wakati.

Kwa upande wa Afisa Sheria kutoka Chama cha Wanasheria Wanawake Zanzibar (Zafela) Khadija Mabrouq Hassan alisema kitendo cha ujenzi wa Baa karibu ya maeneo ya shule hakikubaliki hata kidogo, hivyo aliwaomba wananchi kuungana kwa pamoja kuweka pingamizi ya utolewaji wa vibali muda utakapowadia.

Alisema anaamini wazi kuwa pingamizi za wananchi zinaweza kushinda kutokana na mapangamizi yao yanweza kuwa na mashiko makubwa hasa kutokana na Baa hizo kuwa karibu ya Shule za wanafunzi.

Baadhi ya wamiliki wa Baa hizo walidai kuwa wamekua wakifanya jitihada mbali mbali za kuhakikisha Baa hizo hazina athari kwa watoto, wakidai kuwa kutokana na jitihada hizo ndio maana huopatiwa vibali vya kuendelea na biashara hiyo.

Viongozi wa Serikali wasema

Naye kaimu Sheha wa Shehia hiyo, Suleiman Ameir Juma alisema uongozi wa Shehia hiyo upo tayari kushirikiana na wazazi na wananchi wa eneo hilo katika kuhakikisha suala la elimu kwa watoto linathaminiwa kwa maslahi ya jamii na taifa kwa ujumla.

Alisema katika kulitilia mkazo suala hilo uongozi wa Shehia kwa kushirikiana na wananchi umepanga utaratibu wa kuwaendeleza na masomo ya elimu mbadala wanafunzi 250 walioacha masomo katika kijiji hicho chenye wakaazi 4,250.

Kwa upande wa Afisa Wanawake Wilaya ya Kusini, Haji Choum Haji alisema kutokana na uwepo wa hali hiyo wamekuwa wakifanya jitihada mbali mbali, ikiwamo kutoa elimu kwa watoto, kukaa na wadau mbali mbali, kuzungumza na wazazi pamoja na kutumia njia mbali mbali ili kuona watoto wanaishi katika mazingira bora.

Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja, Ayoub Mohamed Mahmoud akizungumzia kadhia hiyo alisema ni kweli serikali imekuwa ikitoa vibali vya uendeshaji wa Baa, ila wananchi nao wana haki ya kupinga Baa hizo kila muda unapofika wa kuomba vibali kwa wafanyabishara hao.

Alisema kwa upande wa Serikali ya Mkoa huo baada ya kubaini tatizo hilo wameamua kuunda kamati ndogo ya usalama ili kukagua pamoja na kutoa mapendekezo yao kwa kamati ya Mkoa ya usalama ili kama kuna hatua za kuchukua ifanyike hivyo kwa mujibu wa sheria.

Alisema hawafurahii hata kidogo kuona hivi sasa Mkoa wa Kusini kuwa ni moja ya Mkoa unaoasemeka vibaya juu ya athari za watoto ikiwamo kujiingiza katika vitendo vya ngono.

Kwa upande wa Mkurugenzi Elimu ya Maandalizi, Msingi na Kati Safia Rijali alisema tayari Wizara yake imepokea malalamiko kutoka kwa wananchi wa Wilaya hiyo juu ya uwepo wa kadhia hiyo na kuahidi kuwa hatua madhubuti zitachukuli za ufatiliaji.

Alisema si jambo la kupendeza hata kidogo kuona ujenzi wa Baa kuwepo maeneo ya karibu na Shule, akidai kuwa kufanya hivyo ni kuathiri sana sekta ya elimu hasa kwa watoto walio karibu na Baa hizo ambazo kiukweli zinaweza kuduma elimu pamoja na kupeleka kuvunjika kwa maadili kwa watoto.

Makala imeandaliwa na Haji M. Mohd, chini ya ufadhili wa UNICEF

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top