Zanzibar ni miongoni mwa nchi iliyojaaliwa neema ya bahari nzuri na yenye kuvutia ambayo wananchi wake pamoja na serikali kwa ujumla wamekuwa wakiitumia katika shughuli mbali mbali za kijamii, kiuchumi na maendeleo.

Miongoni mwa shughuli ambazo hutumika kupitia uwepo wa bahari visiwani hapa ni pamoja na uvuvi, kilimo cha mwani, Utalii pamoja na shughuli nyengine mbali mbali zenye kuingiza kipato kwa jamii na taifa.

Licha ya habari kutumika kwa matumizi mbali mbali, lakini matumizi makuu ya bahari visiwani hapa ni uvuvi ambao hutoa fursa kubwa hasa kwa wananchi wanaoishi maeneo ya karibu na habari au wakati mwengine hata waishio maeneo ya mbali.

Hii ni moja ya fursa ambayo imekuwa ichangamkiwa kwa kasi hasa na vijana wanaoishi pembezoni mwa bahari, kutokana na utendeaji kazi wake hauhitaji elimu ya shule, chuo au utaalaam ambao upatikanaji wake huwa mgumu kwa wanyonge.

Ni vijana wengi wamekuwa wakinufaika na matumizi ya bahari ambapo baadhi yao kupitia kazi ya uvuvi hawatamani hata kazi nyengine, kutokana na uingizaji wa kipato chake huwa ni kikubwa ukilinganisha na baadhi ya kazi nyengine za kawaiada.

Hakuna asiyefahamu kwamba kazi ya uvuvi imegawika katika maeneo mbali mbali, wapo wavuvi, madalali wa kuuza samaki, wanunuzi pamoja na wahudumu wa mwisho ambao ni waparaji samaki baada ya wanunuzi kununua.

Kwa kuwa kazi ya uparaji wa samaki kuonekana ni kazi ya mwisho kabisa katika sekta ya uvuvi, imeonekana ni jambo la kawaida katika maeneo mbali mbali visiwani hapa watoto walio chini ya miaka 18, ndio wahusika wakuu wa uparaji wa samaki.

Ni maeneo mengi hasa katika masoko ya samaki vijijini watoto ni wahusika wakuu wa kazi hiyo, ikidaiwa kuwa hali hiyo husababishwa na kipato cha uparaji wa samaki kuwa ni kidogo, hivyo kazi hiyo mara nyingi huwaachiwa watoto .

Baadhi ya watoto hufanya kazi hiyo huku wazazi au walezi wao wakitambua au wakati mwengine wao ndio huwa wasimamizi wakuu wa kuona watoto wao wanapata kazi nyingi ili kupusha suala la kuombwa pesa ovyo na vijana wao hao.

Licha ya wazazi hao kuona wanachofanya kuwa ni sahihi kwa maslahi yao dhidi ya watoto hao, lakini ukweli ni kwamba kufanya hivyo ni kuwadumaza watoto kiakili pamoja na kuwaandaliwa maisha mabaya hapo baadae, kwani baadhi ya watoto hao shule wamekatisha.

Ni mara nyingi sana tumekuwa tukisikia malalamiko ya walimu wa shule hasa kwa shule zilizopo karibu na bahari, wakidai kuwa utoro pamoja na ukataji wa masomo kwa watoto wa maeneo hayo yamekuwa ni mambo ya kawaida.

Huku wazazi wao wakiwa hawana hata wasi wasi juu ya watoto, licha ya juhudi kubwa kuchukuliwa na walimu kuitisha vikao mara kwa mara ili kujadili mustakabali mzuri juu ya utoaji wa elimu kwa watoto.

Ifahamike kwamba licha ya wazazi kuona kufanya hivyo ni kuwapenda watoto au kuwapa mbinu za kutafuta pesa mapema, lakini njia hiyo ni kuwapotosha watoto na kuwaandalia mazingira mabaya katika maisha yao ya baadae.

Umefika wakati sasa kwa wazazi, taasisi mbali mbali za wanaharakati pamoja na serikali kwa ujumla kushirikiana kwa pamoja katika kulifanyia kazi suala la watoto kutoshirikia kazi ya uparaji wa samaki, ili kuona watoto hao wanaandaliwa vyema ili kuja kuwa viongozi wazuri wa familia, au serikali hapo baadae.

Licha ya taasisi mbali mbali kikiwamo cha Waandishi wa habari za Maendeleo Zanzibar (Wahamaza) Shirika la Kimataifa la kuhudumia watoto (Unicef) kufanya kazi kuwa ya kutoa elimu juu ya umuhimu wa elimu na malezi bora kwa watoto, lakini bado wazazi wana haki kubwa ya kuona watoto wao wanaishi katika mazingira bora.

Tunaamini hilo linawezekana pindi kila mmoja akatambua umuhimu wa kuwatunza na kuwalea watoto katika makuzi bora hasa ya kielimu ni jukumu la kila mmoja, ili baadae kuja kufurahia matunda ya kuwa na wataalam wenye sifa nzuri kutoka ndani ya nchi badala ya kuwa na wataala kutoka nje ya nchi.

Imeandiliwa na Haji M. Mohd, chini ya ufadhili wa UNICEF

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top