Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

LICHA ya uwepo wa malalamiko kwa baadhi ya wananchi wanaodai kukosa kuandikishwa katika daftari la wapiga kura, kwa sababu mbali mbali, Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) imesema tathmini kamili ya zoezi zima inatarajiwa kufanyika baada ya zoezi hilo kukamilika.

Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jaji Mkuu Mstaafu Hamid Mahmoud Hamid alitoa kauli hiyo katika muendelezo wa zoezi hilo linaloendelea huko kaskazini Unguja kwa Wilaya ya Kaskazini ‘’A’ na ‘B’.

Alisema baada ya kukamilika kwa zoezi hilo tume itafanya tathmini ili kuangalia kwa namna ambavyo itaweza kusaidia kuzitatua changamoto za Wananchi ambao wamekosa fursa ya kuandikishwa katika Daftari kutokana na sababu mbali mbali ikiwamo ya kukosa Vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi.

Alisema kutokana na uwepo wa malalamiko hayo uongozi wa tume hufanya ziara katika vituo kwa kupata tathmini ya awali ili kujua mafanikio na changamoto juu ya utaratibu wa uandikishaji na uhakiki wa taarifa za wapiga kura unavyoendelea.

Kwa upande wa mwanasheria mkuu wa zamani wa Zanzibar, Abubakar Khamis Bakary alisema zoezi la Uandikishaji katika Daftari la kudumu la Mpiga kura, linashangaza sana kuona Tume inakataa kuwaadikisha wananchi ambao hawajapatiwa kitambulisho kipya cha Mzanzibar mkaazi, lakini vitambulisho vya zamani wanavyo.

Alisema kufanya hivyo ni kuwanyima haki wananchi, huku akiweka wazi kwamba ACT wataendelea kudai haki ya wananchi wake, ili kuona kila mwananchi anaandikishwa kwa mujibu wa sheria za nchi.

Hata hivyo Abubakar alidai kuwa watendaji wa ofisi ya Vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi kwa kushirikiana na tume ya uchaguzi Zanzibar (ZEC) hawana nia njema na ndio maana hadi leo hii wananchi walio wengi hawana vitambulisho.

Hata hivyo kwa upande wa Mkurugenzi Wakala wa Matukio ya Kijamii Zanzibar, Dk Hussein Khamis Shabani hivi karibuni alisema ukosefu wa vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi kwa baadhi ya wananchi kunatokana changamoto za kukosewa kwa baadhi ya taarifa za wananchi hao na si vyenginevyo.  

Alisema waliokosa vitambulisho hivyo kwa awamu ya kwanza wasiwe na hofu na kwamba kila mtu aliekidhi vigenzo vya kisheria vya vya kupatiwa kitambulisho hicho ajue atapatiwa bila ya usumbufu wowote.

Kwa upande wa Mkurugenzi wa uchaguzi  Zanzibar (ZEC) Thabit Idarous Faina alisema wao kama tume ya uchaguzi (ZEC) hawahusiki na utoaji wa vitambulisho na kwamba kinachowahusu wao ni uandikishaji wa piga kura wapya na uhakiki kwa wale wote wa zamani.

Faina alisema alisema Tume ya Uchaguzi itamuandikisha kila mwananchi aliyetimiza sifa za kuandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa mujibu wa Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar Nam. 4 ya mwaka 2018 ili kuweza kupiga kura katika Uchaaguzi Mkuu wa 2020.

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top