Na Mwandishi Wetu, Zanzibar


Afisa Uandikishaji Wilaya ya Kaskazini “B” MAKAME PANDU KHAMIS alisema zoezi la Uandikishaji wa Wapiga Kura Wapya na uhakiki wa taarifa za Wapiga Kura linaendelea vizuri katika Vituo vyote vya Wilaya ya Kaskazini “A” na vituo vya Shehia za Jimbo la Donge.

Akizungumza wakati akitembelea vituo hivyo, Afisa huyo alisema zoezi hilo linaendelea vizuri kutokana na maandalizi na juhudi zinzochukuliwa na Watendaji wa Tume pamoja na Masheha wa Shehia kuhamasisha Wananchi wao kwenda katika vituo kujiandikisha na kuhakiki taarifa zao.

Aliongeza kusema kuwa, mpaka sasa Vituo vyote 33 vya Wilaya ya Kaskazini “A” pamoja na Vituo tisa vya Jimbo la Donge kuna Idadi Kubwa ya Wananchi waliojitokeza kuandikishwa na kuhakiki taarifa zao mbali na baadhi ya changamoto ndogo ndogo zilizojitokeza vituoni ambazo zilirekebishwa kwa kupewa maelekezzo wapiga kura kwenda katika vituo ambavyo zipo taarifa zao.

Aidha, Ndugu Makame alieleza kuwa amani na utulivu umetawala katika Vituo hivyo ambapo aliwataka wananchi hususan Vijana ambao wametimiza sifa za kuwemo kwenye daftari kwenda kujiandikisha na kwa wale waliokuwemo katika Daftari kwenda kuhakiki taarifa zao kwani bila kufanya hivyo hawatoweza kupiga kura kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.

Nao baadhi ya Mawakala wa vyama vya Siasa katika vituo mbali mbali vya Uandikishaji vya Wilaya hiyo walisema uandikishaji na uhakiki wa taarifa za Wapiga kura ni jambo la kitaifa hivyo, kuna kila sababu ya kila mwananchi kwenda kujianddikisha ikiwa ni hatua moja wapo ya kukuza Demokrasia nchini.

Wananchi ambao walifika katika vituo kuomba kuandikishwa pamoja na kuhakiki walisema utulivu katika maeneo hayo umewavutia zaidi kwenda katika vituo hivyo ambapo wamewaomba wananchi ambao hajaandikisha wafanye hima kutumia fursa hiyo kabla ya muda uliopangwana Tume kumalizika.

Zoezi la uandikishaji wa Wapiga Kura Wapya na uhakiki wa taarifa za Wapiga Kura waliokuwemo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa Wilaya ya Kaskazi “A” na Jimbo la Donge unatarajiwa kumalizika Siku ya Jumatano ya tarehe 19/2/2020

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top