WANAWAKE wana mchango
mkubwa katika kutekeleza majukumu ili kuziimarisha familia zao.
Akizungumza katika
maadhimisho ya ‘Siku ya Wanawake Duniani’ yaliyofanyika jana Machi 8, 2018
katika kijiji cha Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja, mke wa Rais wa Zanzibar
Mama Mwanamwema Shein, amesema wanawake ni nguzo muhimu ya kuinua familia.
Amesema akinamama
wana mchango mkubwa katika kuimarisha familia ili zipate ustawi na kuzifanya
zipige hatua zaidi ya maendeleo nchini.
Hata hivyo, ameeleza
kuwa wanawake na watoto ndio waathirika wakubwa kila kunapotokea matatizo
nchini yenye mwelekeo wa kupoteza amani.
Kwa hivyo amesisitiza
haja ya kuendeleza ushirikiano katika kuendeleza amani na mshikamano ili
kuhakikisha wanawake na watoto wanakuwa salama na kuishi bila khofu.
Aidha, Mama Shein
aliwataka akinamama na akinababa kushirikiana katika malezi bora ya watoto
kulingana na maadili, silka na utamaduni wa nchi ili wawe raia wema.
Kuhusu vitendo vya
udhalilishaji wa kijinsia vinavyoendelea kushamiri kwa kasi, Mama Mwanamwema
alisema Zanzibar bila ya uovu huo unaoathiri maendeleo ya taifa inawezekana
iwapo jamii itakuwa kitu kimoja kwa kushirikiana kuvikomesha
Sambamba na hayo,
alisema katika kupinga mapambano dhidi ya maradhi ya ukimwi, wanawake wana
mchango mkubwa wa kudhibiti maambukizo ya virusi ifikapo mwaka 2030.
Lakini alieleza
kusikitishwa kwake na kiwango kikubwa cha wanawake wanaoambukizwa maradhi hayo
ambako kiko juu kuliko kwa wanaume.
“Takwimu zinaonesha
kuwa idadi ya wanawake wanaoishi na virusi vya ukimwi nchini ni mara mbili ya
wanaume, hivyo tuchukuwe hatua madhubuti za kujiepusha na vitendo
vinavyochangia kupata maradhi hayo,” alisisitiza.
Aidha aliwataka
wanawake kuzitumia fursa za kujiunga na vikundi vya ushirika ili kujiimarisha
kiuchumi kwa kujiongezea kipato na kupambana na umasikini, hali itakayoipa
nguvu Serikali na washirika wengine kutanua wigo wa misaada yao.
Kwa upande wake,
Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake na Watoto Mhe. Maudline Cyrus
Castico, alisema wakati umefika kwa wanawake kushirikiana katika kuleta
mabadiliko vijijini ili kufikia ukombozi wa kiuchumi.
Alieleza kuwa,
wanawake wana nafasi kubwa ya kuleta maendeleo nchini, hatua inayoweza
kuwafanya wajielewe na kujitambua.
Castico alikemea
tabia iliyoanza kujitokeza sasa ambapo baadhi ya watu na makundi huwakamata
wanawake na watoto, kuwapiga na kuwafanyia vitendo vya udhalilishaji ikiwemo
kuwabaka.
Siku ya Wanawake
kimataifa, iliasisiwa na Umoja wa Mataifa kupitia mkutano uliofanyika mwaka
1995 jijini Beijing China, ambapo ujumbe wa mwaka huu ni, “Wakati umefika
tushirikiane kuleta mabadiliko ya wanawake vijijini”.
Mwisho
Facebook Blogger Plugin by Piere
Post a Comment