Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) inapenda kutoa Taarifa kwa Wananchi juu ya upungufu wa Mafuta ya Petroli uliyojitokeza katika Vituo vya Mafuta vya Kampuni ya United Petroleum (UP) na kusababisha Foleni katika Vituo vya Mafuta vya Kampuni za Zanzibar Petroleum (ZP) na GAPCO.

Meli ya ‘United Spirit 1’ ya Kampuni ya United Petroleum (UP) imefanikiwa kupakia Mafuta ya Petroli Lita 1,820,000 (1400 Metric Tones) jana Mchana tarehe  23/02/2018 katika Bandari ya Dar es salaam, na Meli hiyo inatarajiwa kufika Zanzibar Leo Usiku na kushusha Kesho Asubuhi.

Aidha, Meli ya ‘MT Ukombozi’ ya Kampuni ya GAPCO nayo inatarajiwa kupakia Mafuta ya Petroli Lita 1,170,000 (900 Metric Tones) na Dizeli Lita 1,080,000 (900 Metric Tones) Kesho Jumamosi 24/02/2018 katika Bandari ya Dar es salaam na inatarajiwa kufika Zanzibar Kesho Usiku na kushusha Keshokutwa Asubuhi.

Ni matarajio ya ZURA kuwa kufikia Jumatatu tarehe 26/02/2018 upatikanaji wa Mafuta Zanzibar utakua umerejea katika hali ya kawaida, hivyo Wananchi wanaombwa kuendelea kuwa wastahamilivu katika kipindi hiki kigumu.

Pia ZURA inaendelea kusimamia zoezi la usambazaji na uuzwaji wa mafuta vituoni kwa yale yaliyopo mpaka Mafuta yaliyoagizwa yatakapofika nchini na kuhakikisha yanauzwa kwa mujibu wa maelekezo ya Mamlaka.

ZURA inaomba ushirikiano kutoka kwa Wadau wote wa Mafuta na Wananchi katika kukabiliana na changamoto hii.

IMETOLEWA NA KITENGO CHA UHUSIANO (PRU)
MAMLAKA YA UDHIBITI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI ZANZIBAR (ZURA)

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top