MWENYEKITI wa Kamati ya Kusimamia Viongozi Wakuu wa Kitaifa ya Baraza la Wawakilishi, Omar Seif Abeid, ameishauri Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, kufuatilia mgao wa tozo la minara ya kuongozea meli linalofikia shilingi 1 bilioni ambalo halijalipwa.

Alitoa ushauri katika kikao cha baraza la wawakilishi kinachoendelea wakati akiwasilisha ripoti ya kamat hiyo kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

Alisema endapo watafuatilia deni hilo,serikali itapata mapato yake kwa uhakika.

Aidha alisema ofisi ya uratibu ya SMZ iliyopo Dare es Salaam, imetekeleza wajibu wake wa kuratibu ufuatiliaji wa suala hilo lakini bado halijapatiwa ufumbuzi kati ya taasisi zinazohusika.

Aidha alieleza kuwa takriban miaka miwili sasa serikali imekuwa ikidai deni hilo la asilimia 41 za mgao ambapo Tanzania Bara inapata asilimia 59.

Hata hivyo, kamati imeshauri wizara  kutoa miongozo maalum kwa wizara na taasisi zote za serikali juu ya umuhimu wa kuitumia ofisi ya uratibu wa shughuli za SMZ iliyopo Dare es Salaam, kabla maofisa na watendaji wao kuanza kazi huko.

Akizungumziatume ya uratibu wa udhibiti wa dawa za kulevya, aliishauri tume hiyo kuhakikisha wanaimarisha mazingira ya bandarini ikiwa ni pamoja na kuweka wataalamu na vifaa vya kutosha vya uchunguzi.

Akizungumzia tume ya uchaguzi, alisema kamati yake imebaini baadhi ya kasoro zinazoikabili tume hiyo.

Alitaja miongoni mwa kasoro hizo kuwa ni uhaba wa vyombo vya usafiri hasa magari, ukosefu wa majengo ya kudumu ya wilaya na ukosefu wa ghala la kuhifadhia vifaa.

Kuhusu kamisheni ya kukabiliana na maafa, alisema licha ya kuwa inatekeleza majukumu yake, lakini kamati imebaini changamoto ikiwemo uhaba wa bajeti unaosababisha kuacha kutekeleza baadhi ya shughuli.

Alisema Tume ya Ukimwi pia inapaswa kuendelea kuihamasisha jamii kufanya uchunguzi wa saratani ya kizazi mara kwa mara hususan watu wanaoishi na VVU ambao wamo katika hatari ya kupata ugonjwa huo.

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top