Wakati Mwenyekiti wa Cuf anayetambulika na msajili wa vyama vya siasa Tanzania Profesa Lipumba leo akiwa ndani ya kisiwa cha Pemba kwa ajili ya Mkutano na wafuasi wa Chama hicho, upande unamuunga mkono katibu Mkuu wa Chama hicho waja juu na kutoa tamko lifuatalo.


TAARIFA RASMI YA CHAMA CHA WANANCHI-CUF KUHUSU UJIO WA IBRAHIM LIPUMBA KISIWANI PEMBA.



CUF - Chama cha Wananchi kimepokea taarifa ya ujio wa Ibrahim Lipumba kisiwani Pemba siku ya Jumamosi tarehe 24 Februari 2018, kutoka kwa Mkuu wa Polisi Wilaya ya Chake Chake Pemba kwa barua yake ya tarehe 23 Februari 2018 kwa Ofisi ya Wilaya ya CUF Chake Chake.

Makao Makuu ya CUF Zanzibar haijapeleka barua yoyote kuhusu ujio wa Lipumba kwa Jeshi la Polisi kama inavyodaiwa na barua hiyo ya Polisi.

CUF - Chama cha Wananchi kinatambua kuwa Lipumba sio kiongozi na wala sio mwanachama wa CUF baada ya kufukuzwa rasmi na Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.

Chama cha Wananchi - CUF kinaamini kuwa ziara hiyo ni uchokozi wa makusudi unaofanywa na kibaraka Lipumba akishirikiana na Jeshi la Polisi. Ziara hii imekuja baada ya kufeli Jaribio la uvamizi wa Makao Makuu ya CUF Mtendeni ambalo lilikuwa na dhamira ovu sana kwa Chama.

Lengo la ziara hii ni kuwafanya wananchi, kama lilivyokuwa lile la uvamizi wa Makao Makuu Mtendeni, kututoa katika kupigania haki yao ya Ushindi Mkubwa iliyoporwa baada ya Uchaguzi wa tarehe 25 Oktoba 2015.

Chama cha Wananchi-CUF kinawataka wanachama, viongozi na wapenzi wa CUF waliopo Pemba kuwa watulivu kuendelea na shughuli zao za maisha za kawaida na kupuuza kabisa ujio huo wa Lipumba.

Kama tulivyoshinda uchokozi wa kuvamiwa Makao Makuu Mtendeni tukashinde tena kwa kutokukubali kutolewa katika mstari kupitia uchokozi huu anatumiwa kibaraka Lipumba kupitia ziara yake hii ya Pemba.

HAKI SAWA KWA WOTE
Nassor Ahmed Mazrui
Naibu Katibu Mkuu
Zanzibar

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top