RAIS wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS), Omar Said  Shaabani, amesema tatizo la kuchelewa kwa kesi za jinai zinazohusiana na udhalilishaji, inatokana na jamii kutokuwa tayari kwenda kutoa ushahidi mahakamani.

Aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na Zanzibar Leo baada ya kufunguliwa mahakama ya wilaya Mwanakwerekwe.

Alisema tabia ya watu kutokwenda kutoa ushahidi ni kikwazo kikubwa jambo  ambalo linasababisha mahakama huwaachia huru washtakiwa kwa sababu ushahidi huwa haukamiliki.

“Kesi nyingi zinafikishwa mahakamani lakini ushahidi ndio unaomfanya mtuhumiwa atiwe hatiani, ila kwa sasa jamii inaogopa kwenda kutoa ushahidi hali inayosababisha washtakiwa kuachiwa huru,” alisema.

Aidha tatizo jengine, watu wanapenda kumalizana kifamilia hali ambayo mahakama inapata wakati mgumu kushughulikia kesi hizo.

Akizungumzia majengo ya mahakama, alisema serikali iko mstari wa mbele kuzifanyia matengenezo mahakama mbalimbali zilizopo nchini ili kuwapa furaha ya kufanya kazi watendaji.

“Tumeona serikali ikiziimarisha mahakama zetu, naamini na mahakimu watafanya kazi vizuri kwa mujibu wa sheria,” alisema.

Alitoa wito kwa wananchi kufika mahakamani kutoa ushahidi kwani kesi bila ya ushahidi haziwezi kupata hukumu.

Juzi Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu, alisema ofisi yake haitawavumilia mawakili wanaoahirisha kesi bila sababu za msingi na kusababisha kesi hizo kuchukua muda mrefu kutolewa hukumu.

Alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika hafla ya  kukabidhi vyeti kwa mawakili wapya, iliyofanyika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni.

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top