Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja  Mhe. Hassan Khatib Hassan amesema serikali mkoani humo itaendelea kusimamia vyema agizo lililotolewa na Rais wa Zanzibar Dk. Ali Moh’d Shein la kudhibiti biasharaa ya magendo.

Mhe. Khatib ametoa kauli hiyo afisini kwake tunguu katika kikao cha pamoja kilichowashirikisha  maofisa kutoka mamlaka ya usafiri baharini, bodi ya mapato Zanzibar, KMKM, wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa chenye lengo la kutafuta ufumbuzi wa vyombo vinavyokamatwa na magendo mkoani humo.

Amesema kufuatia kushamiri kwa biashara hiyo serikali ya mkoa huo imedhamiria kupanga mikakati ya pamoja na taasisi hizo itakayoweza  kukomesha  biashara hiyo ambapo amezisisitiza taasisi hizo kuwa makini katika kusimamia dhamana zao.

Amesema serikali haina lengo la kuwakomoa wananchi katika kupambana na vitendo hivyo bali inataka kuona kwamba kila mwananchi anafuata sheria na taratibu za kutumia bandari zilizo rasmi katika kusafirisha bidhaa zao.

Nae mkurugenzi wa ulinzi na usalama mamlaka ya usafiri baharini Capt, Msilimiwa Idd Juma amewataka wamiliki wa vyombo vya baharini kuona umuhimu wa kufuata sheria na taratibu za usajili wa vyombo vyao ili kuepukana na athari mbali mbali zinazoweza kujitokeza.

Mnamo mwezi wa august mwaka jana Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa baraza la mapinduzi Dk. Ali Moh’d Shein aliuagiza uongozi wa serikali mkoa wa kusini unguja kulipatia ufumbuzi tatizo la utumiaji bandari bubu katika kuendesha biashara za magendo.

Chanzo, Zanzibar 24

Facebook Blogger Plugin by Piere

Post a Comment

 
Top